Na. Mwandishi Wetu – Geneva
Serikali ya Tanzania na Marekani zimeanza mazungumzo ya kuandaa mkataba mpya wa ushirikiano wa afya unaolenga kuwa mfano kwa nchi nyingine za Afrika, huku ukiahidi kuimarisha usalama wa afya, bima ya afya kwa wote na uzalishaji wa ndani wa bidhaa tiba.
Hatua hiyo imefikiwa leo Jumatatu, Mei 18, 2026 mjini Geneva nchini Uswisi, katika mkutano kati ya Waziri wa Afya wa Tanzania, Mohamed Omary Mchengerwa na Ofisa wa Marekani wa Shirika la Global Health, Brad Smith.

Katika mkutano huo, pande zote mbili zilikubaliana kuharakisha majadiliano kuhusu pendekezo la hati ya makubaliano ya ushirikiano wa afya ya kimataifa kati ya Tanzania na Marekani, huku zikisisitiza kuwa ushirikiano huo unapaswa kuwa na manufaa kwa pande zote na kuzingatia sheria za kitaifa pamoja na wajibu wa kimataifa.
Smith anahudumu kama Mshauri wa Masuala ya Afya Kimataifa na Mshauri Mwandamizi katika Ofisi ya Usalama wa Afya ya Kimataifa na Diplomasia ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani.

Mazungumzo hayo yalifungua ukurasa mpya wa ushirikiano wa afya kati ya nchi hizo mbili, huku Tanzania ikiweka wazi dhamira yake ya kujenga mfumo imara zaidi wa afya unaojitegemea na wenye uwezo wa kukabiliana na changamoto za kiafya za sasa na zijazo.
Akizungumza katika mkutano huo, Mchengerwa amesema Tanzania ina matumaini makubwa kuhusu mazungumzo hayo na iko tayari kuanza ushirikiano wa kiufundi.






