CCM Mkoa wa Iringa waridhishwa na utekelezaji wa miradi

Kamati ya Siasa ya Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Iringa imeridhishwa na utekelezaji wa Mradi wa Skimu ya Umwagiliaji ya Mkombozi uliopo Tarafa ya Pawaga, Wilaya ya Iringa, unaotekelezwa na Serikali kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 56.

Mradi huo, unaolenga kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo, kuimarisha usalama wa chakula na kuinua uchumi wa wananchi wa eneo hilo, umefikia asilimia 95 ya utekelezaji na unatarajiwa kukamilika pamoja na kukabidhiwa rasmi mwezi Septemba mwaka huu.

Akizungumza wakati wa ziara ya Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Iringa ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo wilayani humo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Iringa, Daud Yassin, amewataka wananchi kuwa walinzi wa miundombinu ya mradi huo kwa kuitunza na kuilinda ili idumu na kuendelea kuwanufaisha wananchi pamoja na vizazi vijavyo.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James, amesema Serikali imewekeza katika ukanda wa Pawaga kupitia mradi huo wa umwagiliaji kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa chakula na kuimarisha usalama wa chakula nchini.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Skimu ya Umwagiliaji Mkombozi, Chesco Msamba, amesema mradi huo umeleta matumaini mapya kwa wakulima kwa kuondoa changamoto ya utegemezi wa mifereji ya asili ya umwagiliaji, huku ukitarajiwa kuhudumia zaidi ya ekari 15,000 za mashamba.

Baadhi ya wananchi wanaonufaika na skimu hiyo wamesema mradi umeongeza fursa za kilimo cha uhakika, umewezesha uzalishaji wa mazao kwa mwaka mzima na kuboresha kipato pamoja na maisha yao kupitia shughuli za kilimo.

About The Author

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *